Mdhamini Mkuu wa Ligi Kuu ya
Vodacom Tanzania bara (VPL), Kampuni ya Mawasiliano ya Vodacom Tanzania, jana ilivikabidhi vilabu 16 vitakavyoshiriki ligi hiyo msimu huu kwa
kuzipatia vifaa vipya vya michezo vyenye thamani ya Sh. milioni 490 kwa
ajili ya msimu huu.
Vifaa hivyo vimekabidhiwa jana
katika hafla iliyofanyika jijini Dar es Salaam .Mkuu wa idara ya
Masoko na Mawasiliano wa kampuni hiyo, Kelvin Twisa, akisema kutolewa
kwa vifaa hivyo ni sehemu ya utekelezaji wa matakwa ya kimkataba kati yao na
Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) ili kuhakikisha ligi hiyo inaendeshwa
vizuri
“Kwa niaba ya Vodacom Tanzania,
ninazitakia kila la kheri timu zote 16 zinazoshiriki VPL msimu huu. Timu
bora na ishinde,” amesema Twissa.
Vifaa vilivyokabidhiwa kwa
wawakilishi wa klabu zote 16 ni pamoja na jezi za mechi, jezi za
mazoezi, mipira, viatu, soksi, vilinda ugoko, nguo za kawaida kwa ajili
ya wachezaji na maofisa wa klabu, glavu na vitendea kazi vya waamuzi.
Ofisa Mtendaji Mkuu wa Bodi ya
Ligi Kuu nchini (TPLB), Boniface Wambura, aliushukuru uongozi wa Vodacom
Tanzania kwa kuongeza mkataba wa miaka mitatu wenye thamani ya Sh.
bilioni 6.7 kuendelea kuidhamini ligi hiyo.Wambura aliahidi kuwa bodi hiyo itashirikiana na TFF kuhakikisha ligi inachezwa bila upendeleo kwa baadhi ya timu.
“Timu zimeongezeka kutoka 14 hadi
16, hivyo tutakuwa na mechi 240 msimu huu. Tumejipanga kuhakikisha
tunakuwa na ligi bora kuliko msimu uliopita,” amesema.