Wanafunzi 5,157 wa sekondari wamefukuzwa shule mwaka 2011 kutokana na kugundulika kupata ujauzito.
Hayo yalielezwa jana jijini Dar es Salaam na mratibu wa mafunzo ya jinsia kutoka Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Winifrida Rutaindurwa katika semina ya waandishi wa habari kuhusu changamoto zinazowakabili watoto wa kike.
Akizungumza katika semina hiyo iliyoandaliwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto (UNICEF), alisema idadi hiyo ambayo ni sawa na asilimia 6.8 ni ndogo ikilinganishwa na ya waliobainika kupata ujauzito na kufukuzwa mwaka 2010 ambao walikuwa 5,346 sawa na asilimia 8.1.
Kwa mujibu wa mtaribu huyo, katika utafiti wao wamebaini kwamba vyanzo vikuu vya tatizo hilo ni ukosefu wa usafiri wa uhakika kwa wanafunzi hao hali inayowafanya wengi wao hasa wanaosoma mijini kushawishika na lifti.
Vyanzo vingine ni umbali wa shule na maeneo wanayoishi, ukosefu wa mabweni kwa wanaosoma shule za kutwa na nyingine, matumizi mabaya ya teknolojia ikiwemo televisheni, mitandao ya kijamii kama face book, twiter na vingine.
Alisema ili kuepuka matatizo hayo, ni vyema jamii ikatambua kwamba watoto wa kike pia wanapaswa kupewa fursa kama walivyo watoto wa kiume hasa katika masomo.